Back to Learning Plan
Kufunga Kwa Kuzingatia
Day 6: Mawasiliano ya Kuzingatia
Niliona tangazo nilipokuwa safarini katika London Underground. Tangazo hilo lilisema: “Agiza lenzi za macho sasa kwa senti 20 pekee kwa siku.” Ingawa mimi si mvaaji wa lenzi, pendekezo hilo lilinivutia kwa kuwa lilionekana nafuu kwa wanaozitumia. Hata hivyo, baadaye niligundua kuwa huu ulikuwa mbinu ya kibiashara.
Senti 20 kwa siku kwa kila lenzi haikusikika kama gharama kubwa. Lakini maandishi madogo yaliyofuatana na alama ya nyota (*) yalifafanua: “senti 20 kwa siku kwa kila jicho.” Hii ina maana ya senti 40 kwa siku. Ukizidisha kwa siku 30, gharama inafikia pauni 12 kwa mwezi—ambayo si nafuu tena kwa usambazaji wa lenzi za mwezi mmoja.
Huu mfano unaoshuhudia kuwa tunaishi katika ulimwengu ambapo ulaji na ubepari ni nguvu kuu za uchumi, na makampuni ni wabunifu katika jinsi wanavyouza bidhaa zao.
"Tunamezwa na ulaji."
Katika jitihada za kuwahamasisha watu kununua na kuwashawishi watumiaji kufanya maamuzi ya ununuzi, ningehoji kuwa mara nyingi maudhui ya uuzaji hukaribia kukosa maadili. Masharti muhimu hayawasilishwi waziwazi katika tangazo au kwenye bidhaa yenyewe, na hivyo kumlazimu mtumiaji kuchimba kwa undani ili kufahamu mpango halisi na kile anachonunua kwa hakika.
Kauli ya kimethali ya Kiingereza isemayo, “It does what it says on the tin,” inayomaanisha kuwa kilichoandikwa ndicho unachokinunua, kwa nadra sana huonekana katika uhalisia. Kinaya cha tangazo tulioitaja kama mfano hapo awali, hasa ni kwamba linawalenga watu wenye uoni hafifu, ambao kwa uwezekano mkubwa watapata ugumu wa kusoma maandishi madogo yaliyoandikwa kwa herufi ndogo.
Kwa kurejea mfano huo katika mjadala wa aya hii, Mwenyezi Mungu anawaelekeza waumini kusema neno lililo nyoofu. Neno lililo nyoofu halina jambo lililofichwa; ni la kweli, la uaminifu, na la wazi kabisa.
Imam Al-Alusi anaeleza kwa kina maana na vipengele vya neno lililotumika katika aya hii kwa maana ya “nyoofu” (سديدًا), akisema:
"Neno lililo nyoofu ni kama mshale ulionyooka unapolengwa kuelekea shabaha yake bila kupotoka katika mwelekeo wake." (Ruh Al Ma'ani).
Tunapopamba ukweli kwa maneno matamu au kuficha yale yanayopaswa kuwekwa wazi, huishia kuwapotosha wengine, jambo ambalo ni hatari sana, hususan linapohusu ahadi na majukumu makubwa. Nakumbuka kushughulikia kesi ya mgogoro wa ndoa uliotokana na ukweli kwamba mke hakuwahi kuelezwa kuwa mume wake alikuwa na maradhi ya muda mrefu kabla ya ndoa, na baadaye aligundua hilo kwa bahati mbaya. Vivyo hivyo, mume naye alilalamika kuwa mke wake hakuwa na afya njema ya mwili, jambo alilolifahamu baada ya ndoa. Pande zote mbili hazikufichua mambo haya, hata pale maswali hayo yalipoulizwa kabla ya ndoa.
Huenda, nilipendekeza, kama mambo haya yangedhihirishwa wazi katika mazungumzo ya kabla ya ndoa, pande zote mbili zingepata nafasi ya kukubaliana, kuvumiliana, na kuukubali uamuzi wa Mwenyezi Mungu, badala ya kuyafanya masuala haya kuwa silaha za kulaumiana baada ya ndoa.
Wito wa kusema neno lililonyooka katika aya hii unatokana na kuwa na Taqwa ya Mwenyezi Mungu. Hii ina maana kwamba kauli zetu zinapaswa kuendeshwa na hisia ya kina ya hofu na uwajibikaji, bila kujali kama mazungumzo hayo yanahusu kazi ya ndoto, ndoa, au jambo jingine la maisha.
Akitoa maoni yake kuhusu aya hii, Imam Ibn Kathir anaelezea faida zifuatazo za kusema ukweli:
Mwenyezi Mungu Mtukufu anawaamrisha waja Wake Waumini kuwa na Taqwa ya Allah, yaani kumcha na kumuabudu kana kwamba wanamuona, na kusema neno lililo sawa na lililo nyoofu—yaani neno lisilo na upotovu wala mkengeuko. Anawaahidi kwamba wakifanya hivyo, Atayarekebisha matendo yao, yaani Atawapa mafanikio katika kutenda mema, na Atawasamehe madhambi yao yaliyopita. Na chochote kitakachowatokea siku zijazo, Atawapa msukumo wa kutubu kutokana nacho. (Ibn kathir)
Mwenyezi Mungu atujaalie uwezo wa kusema na watu huku tukimkumbuka Muumba wetu. Hilo litastahikisha msamaha Wake endelevu juu ya madhambi yetu, na Atatupa mafanikio katika kila tunalolifanya, Insha’Allah. Hili ndilo ahadi ya Allah. Je, kuna mpango bora kuliko hii? Hakuna masharti yaliyofichwa—ni ukweli ulio wazi na maneno ya moja kwa moja.
Shirikiana na tafakari hii katika Quranreflect hapa (imechapishwa kwa lugha ya kiingereza)
Ushauri wa kuzingatia: Mtume (rehema na amani zimshukie) alitushauri mambo mawili kuhusu usemi: kusema ukweli hata kama ni mgumu kiasi gani na kukaa kimya wakati hatuna jambo zuri la kusema. Kabla ya kusema neno, jiulize: Je, ni ukweli? Na je, ni zuri? Ikiwa sivyo, basi kaa kimya. (Buluugh al-Maram)
Somo linalofuata linajadili Taqwa na uwazi wa maadili na linajadili aya ya 8:29.