Back to Learning Plan
Lenzi Tano za Kutafakari Qur’ani
Day 12: Lenzi ya Uzoefu Wangu Binafsi (Sehemu ya 3)
“Ninaweza kujifunza nini kutokana na mahusiano yangu na watu wengine, na majukumu niliyoyapitia, ambayo yatanisaidia kuelewa mafunzo na mifano katika Qur’ani?”
Hebu tuanze kwa kutambua umuhimu wa kuishi maisha halisi — kuchunguza, kushuhudia, na kupitia mambo — kisha kuleta uzoefu huo katika usomaji wetu wa Qur’ani. Tayari tulizingatia hili kwa mtazamo wa Ulimwengu wa Qur’ani, lakini pale tulikuwa tukizingatia historia na maumbile. Sasa, tunazingatia uzoefu wa kibinadamu na mahusiano.
Wakati mwingine mimi husema kuhusu Jina “Rabb al-‘Ālamīn” (Mola wa walimwengu) kwamba: kama hujui mengi kuhusu viumbe na unaona ulimwengu kama mdogo sana, basi mtazamo wako juu ya Mola pia utakuwa “mdogo”. Kadri ufahamu wako wa ulimwengu unavyopanuka, ndivyo taadhima yako kwa Muumba na Umiliki wake inavyozidi kuongezeka.
“Uzoefu wa maisha unaweza kunisaidiaje katika safari yangu ya kutafakari?”
Vivyo hivyo,, tunaweza pia kuwa na uelewa mdogo sana wa maisha na undani wake, pamoja na watu na aina za tabia zao. Hapo ndipo tunaweza kukosa mengi yanayoendelea kwa hakika katika simulizi za Qur’ani. Tunaweza kuchukua mambo juu juu, tukidhani kwamba pale wana wa Nabii Ya‘qub (amani iwe juu yake) walipomshutumu kwa upendeleo, basi lazima walikuwa wakisema kweli. Vile vile, bila ufahamu fulani wa michezo ya siasa na mamlaka, tunaweza kuchukua kauli na vitendo vya Waziri (al-‘Azīz) kwa urahisi mno, na kudhani kwamba wanawake wa mjini walikuwa “wakipiga porojo” tu.
Tazama mifano hapa:
quranreflect.com/posts/15525
quranreflect.com/posts/15553
quranreflect.com/posts/15556
(Mifano hii inatokana na kuchanganya Lenzi mbalimbali, ikiwemo Lenzi ya Maneno, Ulimwengu na Uzoefu.)
“Itakuwaje kama nina uzoefu mdogo wa maisha?”
Hatari ya kuwa na “ulimwengu mdogo” wa uzoefu ni kwamba tunaweza kuona mambo nje ya uwiano wake sahihi. Hivyo, tunaposoma kuhusu makafiri na wanafiki, na dunia yetu ni ndogo kiasi tunawajua tu jamaa zetu, inakuwa rahisi sana kuyahamishia maelezo hayo kwa watu wasio sahihi. Ikiwa hujawahi kuishi chini ya dhulma ya kweli, hata wakwe zako wanaweza kuonekana kama “Firauni na majeshi yake” katika mawazo yako!
“Kwa nini ni muhimu kuendelea kurudi kwenye Qur’ani?”
Wakati mwingine, uzoefu fulani wa maisha hutufanya turudi kwenye Qur’ani na kutafakari jambo ambalo hatukuliona kwa mtazamo uleule hapo awali. Ndiyo maana ni muhimu kuendelea kusoma, kuendelea kuishi, na kuendelea kurudi kwenye Maneno ya Mwenyezi Mungu. Acha usomaji wako wa kila siku uwe katika mazungumzo ya moja kwa moja na maisha yako ya kila siku.
“Uzoefu wangu unaongeza thamani gani, ilhali kuna wanazuoni wengi wenye elimu kubwa kuliko yangu?”
Moja ya matokeo mazuri sana ya Lenzi hii ni kwamba wapo watu wanaoweza kuleta uzoefu katika usomaji wao wa Qur’ani ambao hata wanazuoni wa tafsir (mufassirūn) huenda hawana. Sisemi kwamba wanazuoni wanaishi maisha ya kujitenga au upweke, lakini ukweli ni kwamba hakuna mtu mmoja anayeweza kuunganisha utaalamu wa kiufundi na upeo wote wa uzoefu wa kibinadamu: kufanya kazi yenye hadhi kubwa, kupenda na kupendwa, kuvunjika moyo, kulala mitaani, kuwa mzazi, kumpoteza mpendwa, kumtunza mtu mwenye ulemavu, kupambana na misukosuko ya imani, kumpata Mwenyezi Mungu… na mengine mengi zaidi. Yote haya, yanaleta uzoefu maalum na hivyo basi kumpa binadamu fursa pekee ya kutafakari Qur’ani.
Na hii ndiyo mojawapo ya uzuri wa QuranReflect! Ukweli ni kwamba wanazuoni na wengine wanaoendesha QuranReflect wanapenda sana kusoma tafakari zako, kwa sababu tunaamini kwa dhati kwamba kila mtu ana kitu cha kuongeza katika mazungumzo haya. Kujua jinsi aya zinavyopokelewa na watu kutoka nyanja zote za maisha hakutuongezei tu ufahamu wa kile tunachopaswa kufanya kama walezi na waelimishaji, bali pia huongeza uelewa wetu wa Maneno ya Mwenyezi Mungu yenyewe. Kutuambia tu jinsi Qur’ani inavyoingiliana na uzoefu wako binafsi na mambo ambayo WEWE unayajua vizuri zaidi ni jambo lenye kuelimisha sana.